Mke
wa Rais na Mwenyekiti wa WAMA, Mhe. Mama Salma Kikwete assistiza
umuhimu wa elimu katika kupambana na umaskini, Desemba 3, 2010,
Dar es Salaam
Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete, amesema elimu
ni nyenzo muhimu katika kupambana na umasikini, pia amepongeza
ongezeko la taasisi za elimu nchini.
Alisema hayo jana (Desemba 3, 2010) jijini Dar es Salaam, alipokuwa
akizindua mafunzo ya uuguzi katika Taasisi ya A3 ambayo ni taasisi
dada ya shule za Al Muntazir.
Mama Salma, alisema miongoni mwa mambo yanayotofautisha nchi
zilizoendelea na zinachoendelea ni kiwango cha elimu.
“Hii ni kwa sababu utajiri na mali havijileti vyenyewe kwa mtu,
ni matokeo ya mambo mengine ikiwemo elimu. Kiwango cha elimu
na ujuzi ndicho kinachotofautisha nchi zilizoendelea na zile
zinazoendelea,” alisema.
Alifafanua kwamba, kwa kadri kiwango cha elimu, ujuzi na maarifa
kinavyokuwa juu, ndivyo maisha ya watu katika nchi husika yanavyokuwa
bora.
Kutokana na sababu hiyo, alisema, serikali imeamua kuwekeza
katika elimu, na katika hotuba ya kuzindua Bunge hivi karibuni,
Rais Jakaya Kikwete alisisitiza kipaumbele ni elimu.
Mama Salma alisema, ujenzi wa shule za sekondari katika kila
kata, na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ambacho kimeshaanza kutoa
wahitimu, ni uthibitisho wa dhamira ya dhati ya serikali katika
kuinua elimu nchini.
|