Wake
wa Marais barani Afrika wametakiwa kuwaelimisha wanawake ili waweze
kupambana na maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi kutoka kwa mama kwenda
kwa mtoto, Januari 31 2011
Na Anna Nkinda – Addis Ababa, Ethiopia
Wake wa Marais barani Afrika wametakiwa kuwaelimisha wanawake
ili waweze kupambana na maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi kutoka
kwa mama kwenda kwa mtoto jambo ambalo litaweza kupunguza vifo
vya watoto wachanga.
Wito huo umetolewa leo na mke wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
Ban- Ki moon mama Yoo-Soon- Taek wakati akifungua mkutano mkuu
wa wake za Marais Barani Africa (OAFLA) uliofanyika katika ukumbi
wa mikutano uliopo makao makuu ya umoja wa Africa (AU).
Mama Yoo- Soon Taek alisema kuwa vifo vya watoto wachanga vinavyotokana
na maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa
mtoto hivi sasa vimeongezeka hivyo basi ni jambo jema kama wataweza
kufanya kazi kwa pamoja ili kupunguza vifo hivyo.
“Nafasi yenu katika jamii ni kubwa sana hivyo basi kwa kushirikiana
na wananchi mnaweza kupunguza vifo hivyo na kuhakikisha kuwa hakuna
mtoto ambaye atazaliwa huku akiwa amepata maambukizi ya ugonjwa
wa UKIMWI kwani mkiamua kufanya hivyo hakika mtaweza”, alisema.
Pia aliwataka wake hao wa marais kuwawezesha wanawake ili waweze
kukabiliana na hali ngumu ya uchumi jambo ambalo litawasaidia
kujikwamua kimaisha na hivyo kutokuwa katika mazingira ambayo
yatawasababishia kupata maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI.
Akitoa mada katika mkutano huo Dr. Sheila Sisulu ambaye ni Mkurugenzi
Mtendaji wa Shirika la Chakula Duniani (WFP) alisema kuwa shirika
hilo limekuwa likinunua chakula mashambani ambacho kwa asilimia
70 kinazalishwa na wanawake lakini jambo la kushangaza ni kuwa
wanawake hao baada ya kuuza chakula hicho wanakinunua tena kwa
bei kubwa.
Aliendelea kusema kuwa jambo wanalolifanya hivi sasa ni kuwawezesha
wanawake wakulima ili waweze kuuza vyakula wanavyovizalisha katika
shirika hilo kwani watalipwa fedha nyingi ambazo zitawasaidia
kuinua kipato cha familia zao.
Dr. Sisulu alisema, “Ninawaomba muweze kuwawezesha wanawake ili
waweze kununua vyakula na kuuza katika shirika letu kwani watalipwa
pesa nyingi ambazo zitawasaidia kusomesha watoto wao na kutunza
familia zao kwakuwa hakuna ushindani wa kibiashara na soko ni
kubwa”.
“Tunataka kutoa pesa katika mifuko ya wanawake kwani wanawake
wanapokuwa na pesa watoto watasoma na kupata chakula na hivyo
kupunguza umaskini ndani ya familia tofauti na wanaume”.
Alimalizia kwa kusema kuwa ukimsomesha mtoto wa kike utakuwa
umeelimisha familia nzima pia mtoto huyo atachelewa kuolewa na
hivyo kupunguza ndoa za utotoni.
Naye Rais wa umoja huo mke wa waziri mkuu wa Ethiopia Mama Azeb
Zenawi alisema kuwa hivi sasa umoja huo unakabiliwa na changamoto
kubwa ya kupambana na ugonjwa wa UKIMWI kwa wanawake jambo ambalo
linasababisha vifo vya kina mama wajawazito na watoto wachanga.
Changamoto zingine ni upungufu wa vitendea kazi vya kutosha pamoja
na fedha za kutosha ambazo zitawasaidia wanachama wa umoja huo
kuwawezesha wanawake katika nchi wanazotoka.
Mkutano huo ambao umemalizika leo ulihudhuriwa na wake wa marais
kutoka nchi 19 akiwemo Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mama Salma Kikwete.
|