WAMA yasisitiza
umuhimu wa uboreshaji afya Na Elimu Mkoani Pemba Mei 14, 2010
Na Philomena Marijani
Taasisi ya WAMA imesisitiza
umuhimu wa uboreshaji afya na Elimu katika Ziara yake ya Maendeleo
Mkoani Pemba Alhamisi Mei 13 2010. Akikabidhi msaada wa vifaa
vya hospitali katika Hospitali ya Chakechake iliyoko Pemba Mwenyekiti
wa WAMA Mhe. Mama Salma Kikwete alisema kuwa vifo vya akina
mama na watoto bado ni tatizo kubwa visiwani. Alisema kuwa juhudi
za dhati bado zinahitajika ili kuhakikisha kuwa wakina mama
wanajifungua salama.
Aidha aliwapongeza viongozi kwa kujiweka malengo
ya kupunguza vifo vya mama wajawazito kutoka 377 kati ya vizazi
hai 100,000, hadi kufikia 251 na kupunguza vifo vya watoto chini
ya umri wa miaka 5 kutoka 101 kati ya watoto 1000 hadi kufikia
71 kwa mwaka huu.
Vifaa vilivyotolewa ni vifaa vya kujifungulia (Delivery Kit)
(01), vifaa vya operesheni ndogo (caesarean kit)(01) na huwa
vinadawa ya kusafishia (self sterilization), Kifaa cha kuvutia
uchafu kwa watoto wanaozaliwa (Sunction pump) kimoja (01), Toroli
la kubebea vifaa vya huduma wodini (Dressing Troley) (01), Mzani
wa watoto (Infant Scale), Vitanda vya hospitali (2) , Magodoro
(2), na Mashuka (4).
Mwenyekiti wa WAMA pia alitembelea Kituo cha Kazi za Amali-Vitongoji,
ambapo pia aliweza kuongea na wanafunzi wa Skuli ya Sekondari
ya Fidel Castro ambapo alielezea umuhimu wa kazi za kituo hicho
kwa ajira za vijana . Kituo cha Amali kinatoa mafunzo ya ufundi
ya umeme, kompyuta, useremala, Magari, uashi, na bomba.
Katika hotuba yake kwa Wanafunzi aliwasihi wawe makini na masomo
yao na waepuke na mambo yote yanaweza kuwaangusha kitaaluma.
“Jiwekeeni malengo makubwa ya kitaaluma, ili msiishie kufuzu
katika ngazi hii ya mafunzo, na sekondari bali, mfaulu na mpate
sifa zitakazowawezesha kuendelea na kozi za mafunzo zaidi kwa
ngazi ya elimu ya juu na hata ngazi ya vyuo vikuu.” Alisema
Mama Salma.
|