..FOUNDATION NEWS

Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete amezitaka taasisi za fedha duniani kutoogopa kuwakopesha wanawake kwani wamekuwa na sifa njema ya kurejesha mikopo kuliko wanaume

Na Gloria Tesha, Beijing, China .

Mama Salma aliyasema hayo juzi mjini hapa alipokuwa akitoa salamu kwa ufupi katika ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake (Global Summit of Women-GSW) uliofanyika katika ukumbi wa Great Hall of People.

“Ukiwakopesha wanawake, una uhakika wa mkopo kurejeshwa maana anaelewa changamoto zinazomkabili na majukumu aliyonayo katika familia na jamii kwa ujumla, taasisi za fedha wasiogope kuwakopesha wanawake,” alisema Mama Salma.

Katika salamu zake hizo, Mama Salma akiwa mke pekee wa Rais kati wake kadhaa wa marais wa Afrika walioalikwa katika mkutano huo ambao hawajafika mpaka jana, alisema siku zote wanawake wamekuwa hodari kurejesha mikopo na kutekeleza lengo la mikopo kwa wakati hivyo hakuna sababu kwa taasisi za kifedha za kimataifa na katika kila taifa kuogopa kuwakopesha.

Akitolea mfano kwa nchini Tanzania, Mama Salma bila kufafanua zaidi, alisema takwimu zinaonesha kuwa, kati ya wanaume na wanawake wanaokopeshwa fedha kwa ajili ya biashara na miradi mbalimbali, wanawake wamekuwa wepesi kurejesha ingawa imekuwa vigumu kuwakopesha kutokana na hofu ambayo haina umuhimu.

Alisema nchi yoyote inayotaka kufanikiwa kiuchumi, lazima imuweke mwanamke mbele kwa kuwa majukumu yake ni mengi na endapo akipewa mwelekeo, anaweza kuyashughulikia na kuyapatia ufumbuzi.

“Wanawake tulio hapa tunawawakilisha wanawake wenzetu kote duniani,  na kwa bahati sisi hapa tumekuwa katika nafasi za juuu kuliko pengine wenzetu walio wengi, tunapokuwa hapa tujifunze kwa wenzetu waliofanikiwa zaidi ili tunaporejea makwetu tuhakikishe tunamuinua mwananmke mwenzetu kutoka chini hadi afike juu,” alisisitiza Mke wa Rais.

Katika ufunguzi huo uliofanywa kwa viongozi kutoa salamu fupi, uliwashirikisha pia Makamu wa Rais wa Vietnam, Nguyen Thi Doan, Waziri wa Wanawake wa Chile, Carolina Schmidt, Maud Olofsson, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati wa Sweden, Rais wa GSW na Mwenyekiti wa Shirikisho la Wanawake wote wa China (ACWT).

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Vietnam, Thi Doan, alisema akiwa mwanamke, anajivunia kuwa kiongozi kutokana na sera za taifa lake kumuinua mwanamke na kuwataka wanawake kuthubutu kuweza pale wanapopewa nafasi za uongozi, biashara na uchumi .

Aidha pia alisema kutokana na kuwa kundi kubwa linalosakamwa na majukumu pamoja na hatari za maradhi, alisema mataifa hayana budi kuweka mazingira mazuri kuwezesha wanawake kufungua miradi na kukuza kipato chao.

Site Search