Wanaume watakiwa kushiriki katika kupunguza vifo vya mama wajawazito na watoto
Na Anna Nkinda – Maelezo, Kibaha - 04/10/2009
Vifo vya kina mama wajawazo na watoto vitapungua endapo jamii nzima hususani wanaume wataamua kuwapeleka kina mama kliniki kwa wakati na kuwajengea mazingira wezeshi ya kujifungua salama.
Hayo yamesemwa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati alipotembelea kwa nyakati tofuti Zahanati ya Magindu, Kituo cha afya Mlandizi na Kibaha vilivyopo mkoani Pwani.
Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema kuwa wanawake 24 hufariki kila siku kutokana na matatizo ya uzazi hii inamaana kwamba mwamke mmoja anapoteza maisha kila saa.
Kwa upande wa vifo vya watoto wanaofariki chini ya miaka mitano alisema kuwa imeshuka kutoka vifo vya watoto 147 kwa vizazi hai 1000 kwa mwaka 1999 na kufikia vifo 91 kwa vizazi hai 1000 kwa mwaka 2007/8 hii imetokana na juhudi ya kuongeza wigo wa chanyo, kupanua huduma za matibabu chini ya mpango wa IMCI, utoaji wa matone ya vitamini A na utumiaji wa vyandarua vyenye dawa.
"Ninawaomba baadhi ya wananchi wa maeneo haya muachane na mila potofu zinazosema kuwa kujifungulia hospitali ni mwiko bali kuanzia sasa mjue kuwa ni lazima kujifungulia katika vituo vya afya ili mama aweze kupata huduma bora zitakazomwezesha kujifungua salama".
"Ni lazima mtoto apate chanjo mara anapozaliwa na ahudhurie kliniki hadi atakapofikisha umri wa miaka mitano ili aweze kupata huduma bora ya afya", alisema.

Mwenyekiti huyo wa WAMA pia aliwataka wakazi wa maeneo hayo kupunguza kasi ya maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI na idadi ya watoto yatima kwa kuwa waaminifu kwa wapenzi wao kwani kwa kufanya hivyo watalinusuru taifa kutoka kwenye kasi ya maambukizi ya ugonjwa huo pia waende kupima na kujua afya zao.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani Hajati Amina Mrisho alisema kuwa mwaka 2000 vifo vya kina mama wajawazito vilikuwa 242 kwa kila watoto 100,000 waliozaliwa hai. Vifo hivyo vimeongezeka hadi kufikia 300 kwa kila watoto 100,000 waliozaliwa hai mwaka 2007.
Hajati Amina alisema,"Sababu kubwa ya kuongezeka kwa vifo hivyo ni kutopatikana kwa haraka huduma za dharura kama upasuaji kwa kina mama wajawazito wanaoshindwa kujifungua kwa njia ya kawaida hasa kwa wale waishio vijijini hii ni kutokana na ukasefu wa miundombinu, wataalamu wenye ujuzi na ukosefu wa vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyopo vijijini.
Aliendelea kusema kuwa ili kukabiliana na tatizo hilo Mkoa huo kwa kushirikiana na Halmashauri zote zimeamua kuboresha vituo vya afya kwa awamu kwa kujenga vyumba vya upasuaji, maabara, kutoa vifaa tiba na watumishi wa afya wenye utaalamu wa kutoa huduma za tiba, , upasuaji na za maabara kwa wagonjwa wenye matatizo ya dharula wanaoishio vijijini.
Kwa upande wa watoto yatima alisema kuwa idadi yao na wanaoishi katika mazingira hatarishi imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka hivi sasa kuna jumla ya watoto yatima 26,812.
Zahanati hizo zimakabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwa ni pamoja na upungufu wa watumishi wa afya, ufinyu wa bajeti ya afya inayopelekea upungufu wa baadhi ya vitendea kazi, ufinyu wa chumba cha kuzalishia, uhaba wa vifaa kama vile vitanda, magodoro na mashuka, ukasefu wa vifaa vya kuzalishia na vifaa vya kutolea huduma za afya ambavyo vingechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha afya ya kina mama na watoto.
Huduma zinazotolewa katika zahanati hizo kwa wagonjwa wa nje na wanaolazwa ni huduma za mama na mtoto, huduma ya maabara, upimaji wa virusi vya UKIMWI na uzuiaji wa maambukizo ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) toka kwa mama kwenda kwa mtoto na huduma ya magonjwa ya kinywa na meno.
Magonjwa yanayoongoza katika vituo hivyo vya afya ni Maralia, magonjwa ya njia ya hewa, magonjwa ya ngozi, kuharisha, majeraha madogo madogo, nimonia, minyoo, magonjwa ya macho, magonjwa ya ngono, upungufu wa damu, uambukizo wa sikio, uambukizo wa njia ya mkojo (UTI) na uambukizo wa sikio .
Katika Zahanati ya Magindu Taasisi ya WAMA ilitoa magogoro 10, Derivary Kit moja, kitanda maalum cha kujifungulia kimoja, mashuka 20 na Vacuum extractor moja na katika vituo vya Afya vya Mlandizi na Kibaha kwa kila kituo ilitoa mashuka 10, Derivary Kit moja, Kitanda cha kujifungulia kimoja, mashuka matano, Dressing Trolley moja, kitanda cha bulimia kimoja , mashuka 10 na Vacuum Extractor moja.
|